Siachi na sitaacha, univae ubunifu
Nizitunge kwa papacha, kundini niweke tifu
Na mafumbo kuyaficha, ‘siwe mepesi ja difu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, siyo kama najisifu
Ghassani nipa m’bacha, nifunze umakinifu
Hata moja ‘sijewacha, nipa mengi yanikifu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, kutunga kwa unadhifu
Tatunga kila kukicha, japo mawazo hafifu
Nimfikie Mwanacha, kwa tungo kuzisarifu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, kutunga bila ya rafu
Hila zenu sitazicha, maoni yenu machafu
Nikishindwa kuchekecha, Bashiru nipige tafu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, niwezeshe Ya Raufu
Nitumie lugha picha, kasrini waishufu
Itopekechapekecha, Mwana alicheze dufu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, kutunga tungo lufufu
Hata ziumie kucha, sitajali usumbufu
Niwe kama wangu pacha, Dillah kwa umaarufu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Siachi na sitaacha, labda nikiwa mfu
‘tajifikichafikicha, niingie kwenye safu
Sharifa ‘sijejificha, wewe kuti miye dafu
Najijuwa mpungufu, kuandika sitaacha
Othman Ame Hamza
Mfungwa huru
Donge, Zanzibar
0776820608
othame10@gmail.com
WRITER – OTHMAN HAMZA