Kuna banati mzuri, aloumbwa kuumbika
Ulimwengu mashuhuri, kila kona atajika
Urembo na utajiri, kila Mtu amtaka
Alonacho kumpoka
Ana milima kidari, yabusu mbingu kufika
Madini lulu ambari, pengine yasopatika
Apendeza mandhari, kila mtu amtaka
Alonacho kumpoka
Tabia nchiye shwari, hupendeza wote mwaka
Kwa jua la anga zuri, ling’aalo likimweka
Misimuye kuna hari, vuli kipupwe masika
Na mitoye na Machaka
Manukiziye uturi, rihi ya kufurahika
Na mila na desturi, zilizodumu mikaka
Wanamuita fakiri, na mali meyalundika
Alonacho kumpoka
Umbo lake huyu mwari, heba ya kutamanika
Hawataki kughairi, wana kani wameshika
Wataka kumhasiri, mulukiye kumpoka
Alonacho kumpoka
Kuna wengi wenye shari, wamwambao ‘badilika!’
Aache chake kizuri, afate kukengeuka
Ila naye hafikiri, bakunja wanamteka
Alonacho kumpoka
Mrembo nakushauri, mwenye heba Afrika
Usikengeke fikiri, sikubali kukengeka
Wakwandamao si siri, kuna jambo wanataka
Ulonacho kukupoka
Nakwambia tahadhari, yao yatilie shaka
Bora wakwite jeuri, kuliko yatokufika
Waepuke mabepari, wachina na Amerika
Na wote wanokutaka, Mamaangu Afrika.
Copy right:Rashid Mwaguni