Ewe mfuma mipango, kwangu iso mipendezi
Ulokithiri urongo, na sifa za kijambazi
Nakufikisha ukingo, kwangu hutopiga mbizi
Ngoma yako siichezi!
Siichezi Maimuna, ungahamu niwe mumo
Kuihiari hakuna,katu sitokuwa chumo
Kwangu huna la kuvuna, nimeshajifunza somo
Ngoma yako siichezi!
Uwanja wako telezi, sinao imani tena
Utakalo siliwezi, hatunao muamana
Yakomeshe maigizi, mwana mja wa laana
Ngoma yako siichezi!
Ni michochezi midundo, unayoniandalia
Ila ni yenye uvundo, ninavyoikadiria
Itanizulia fundo, kesho nikajajutia
Ngoma yako siichezi!
Sinayo hamu sinayo, ya kuuguza makovu
Nina kimoja kijoyo, kisotindikiwa wivu
Na kwa hayo nionayo, najitanibu na nyavu
Ngoma yako siichezi!
Sishiriki ngoma yako, yenye washirika wengi
Ikanipa hamaniko, mja niso na shilingi
Bora nikae kitako, nijiepushie mengi
Ngoma yako siichezi!
Mtunzi: Jibril Adam
Lakabu: Malenga wa Jangwani. (Abu Sanaya)
Nairobi Kenya.
WRITER – JIBRIL ADAM