Siku ya tua na twika, msi ozi akiona,

Pachimbwa patachimbika, utafukuka na mwina

Siri itabainika, bayana kama mchana

Msi ozi akiona, siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua na twika, akikua nyuki jana

Mrina utaumbuka, mrina uki mrina

Taumwa atafutuka, na sega hataliona

Akikua nyuki jana, siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua na twika, siafu wakiungana

Tawa taabani nyoka, atataataa sana

Shimoni asipotoka, atafa humo naona

Siafu wakiungana, siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua na twika, msi jino kitafuna

Minyama ikichanika, fupa akiliguguna

Genderi talainika, na itatafunwa sana

Siku ya tua na twika, msi jino kitafuna.

 

Siku ya tua na twika, mtu bubwi akinena

Kihutubu na kufoka, yote yalorundikana

Palokombo patanyoka, palopinda kupindana

Mtu bubwi akinena, siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua na twika, mwana akizaa mwana

Jira hizo zitafika, kuwe mkembe hakuna

Ndipo utajua fika, dunia si yako tena

Mwana akizaa mwana, siku ya tua na twika

 

Siku ya tua na twika, kila mtu mbona!? mbona!?

Ndipo watakukumbuka, mambo yatakapobana

Sura zitatebwereka, kwa soni wakisonona

Kila mtu mbona? Mbona? siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua na twika, na wino usipotona

Sipotona kuandika, nikupangie na vina

Utatamani kutaka, nitunge japo sivina

Na wino usipotona, siku ya tua na twika.

 

Siku ya tua ya twika, buriani muungwana

Mwisho wangu ukifika, niwe cha kusema sina

Mdhukuri akiweka, yatamwauni awana

Buriani muungwana, siku ya tua na twika.

 

© Rashid Mwaguni

WRITER – RASHID

Categorized in: