Wake wengine ni jaha, nuru shani ya Manani
Wamejaliwa staha, na utu uso kifani
Nyumba hutia furaha, furaha na farahani
Nuru shani ya Manani, wake wengine ni jaha
Wake wengine mizaha, kwa kujawa na utani
Kwamba kucheka ndo siha, mazidadi si maani
Hata kwa mtu maliha, hugeuka mtu duni
Kwa kujawa na utani, wake wengine mizaha.
Wake wengine ni siha, mume kuwa afueni
Ukipata majeraha, moyo kuwa vidondani
Huukamua usaha, ukapoa mwafulani
Mume kuwa afueni, wake wengine ni siha
Wake wengine silaha, hupambania vitani
Kwa ghadhabu na kariha, na utesi wenye kani
Hulipuka kama zaha, wakati wa Volkani
Hupambania vitani, wake wengine silaha
Wake wengine majuha, wapuuzi nje ndani
Hawakomeki kuhaha, si sekunde si kuruni.
Wape kizuri tufaha, watakitupa chooni
Wapuuzi nje ndani, wake wengine majuha
Wake wengine mashaha, wamebobea fanini
Watungao ufasaha, tungo ziso nuksani
Wamejaliwa nasaha, na busara za waneni
Wamebobea fanini, wake wengine mashaha.
Wake wengine karaha, nuhusi na visirani
Hawadumiki nikaha,hata vyuo ishirini
Kwa nyota yao ya mbweha, kuzururia mwituni
Nuhusi na visiwani, wake wengine karaha.
Awaongoe illaha, walopotoka njiani
Nawaomba msamaha, nilowakwaza moyoni
Imenikoma kariha, nakomeka kikomoni
Wake wengine ni jaha, wake wengine karaha.
Rashid Mwaguni
WRITER – RASHID